Monday, September 16, 2013

MASHINDANO YA MISS LUDEWA 2013 DC AWATAKA WAZAZI KUACHA MILA POTOFU NA KUWARUHUSU WATOTO WA KIKE KUSHIRIKI


MKUU wa Wilaya ya Ludewa katika Mkoa wa Njombe Juma Madaha amewataka wazazi na wananchi wa Ludewa kuacha mila potofu na kuwaruhusu watoto wao hasa wa kike kujiunga na mashindano ya urembo(ulimbwende) kwa kuwa kushiriki mashindano hayo siyo uhuni bali ni sehemu ya ajira sawa na michezo mingine kama vile mpira wa miguu, pete na sanaa nyingine.

Madaha aliyasema hayo jana katika mashindano ya miss Ludewa 2013 yaliyofanyika katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya hiyo ambapo ni wasichana tisa tu ndio walijitokeza kushiriki ukilinganisha na idadi kubwa ya wasichana waliopo katika wilaya hiyo yenye idadi ya watu zaidi ya laki moja na nusu.

Mkuu huyo aliwataja wasichana waliojitokeza kushiriki mashindano haya kuwa ni pamoja na Witness Mgimba, Antonia Haule, Neema Hamisi, Sofia Mtitu na Agness Mtitu. wengine ni Dirisi Ngailo, Trefania Haule,Creria Nyauma na mariam Haule ambao hata hivyo walitumia muda mfupi sana kufanya maandalizi.

Witness Thomas Mgimba (9) kutoka kilimahewa Ludewa mjini ndiye aliyeibuka mlimbwende wa kwanza katika mashindano ya kwanza ya kumsaka miss Ludewa 2013 yaliyofanyika kwa mara ya kwanza Ludewa ambapo alijinyakulia taji na zawadi ya shilingi lakitatu (300,000) zilizoandaliwa na waratibu wa mashindano hayo na shilingi laki mbili (200,000) zilizotolewa na mdau wa mashindano hayo Thobias Lingalangala. Pamoja na kioo cha kujitamia (Dressing table).

Nafasi ya pili ya miss Ludewa 2013 ilichukuliwa na Antonia Haule kutoka kata ya Luana ambaye alijinyakulia zawadi ya radio na jumla ya shilingi laki mbili(200,000) ambapo mshindi wa tatu Neema Ernest Hamisi mkazi wa mtaa wa kanisa mjini Ludewa yeye alijinyakulia stendi ya viatu na shilingi laki moja na nusu(150,000) hata hivyo zawadi hizo haikujulikana zitatolewa lini kwa wahusika.

Kwa upande wao wandaaji na waratibu wa mashindano hayo Abelto Chaula (Maheleni) na Tina Intertaiment kwa pamoja walisema wamekumbana na changamoto nyingi katika mchakato mzima ikiwemo wazazi wengi kutowaruhusu watoto wao kujiunga na mashindano lakini kubwa ikiwa ni pamoja na wadau walioahidi kuchangia kushindwa kutoa michango yao kuwezesha kufanikisha zoezi hilo.

Hata hivyo washiriki wengi wa miss Ludewa 2013 walionekana kushiindwa kabisa kujibu maswali yaliyoulizwa na majaji ipasavyo kutokana na kuwa na uelewa mdogo wa mambo ikiwemo kutokuijua hata wilaya yao ikiwemo raslimali zake huku wengine wakikabiliwa na kuyaona madhara ya kukatisha masomo, hata hivyo wasichana wengi walishindwa kukidhi vigezo ikiwemo kuzuia msichana yeyete mwenye mtoto kushiriki mashindno hayo.

mwisho

No comments:

Post a Comment