Bazil Makungu
WANANCHI wa kata ya
Lugarawa katika wilaya ya Ludewa Mkoani Njombe wameitaka serikali kuharakisha mchakato
wa upimaji wa viwanja katika miji midogo iliyotangazwa hivi karibuni ili waanze
kuviendeleza kwa kujenga nyumba za kisasa sanjari na kuingizia halmashauri
mapato.
Wakizungumza na
gazeti hili walisema kukamilika kwa mchakato huo kutapunguza migogoro ya ardhi
inayoendelea kuwakumba wananchi wa miji hiyo midogo kutokana na watu kuvamia
ardhi ya wengine kwa visingozio vya mipaka.
Ali Ponda mwenyekiti
wa kijiji cha Mdilidili katika kata ya Lugarawa kwa upande wake alisema zoezi
la upimaji viwanja kwa wakati itarahisisha na kuainisha maeneo ya makazi,
malisho, maeneo ya hifadhi na viwanja ya michezo.
Naye Afisa mipango
miji wilaya ya Ludewa Isack Makinda alisema eneo la mipango miji la Lugarawa ni
miongoni mwa maeneo matano ya kimpango miji katika wilaya ya Ludewa na kuyataja
kuwa ni pamoja na kata ya Ludewa, Mlangali, Mawengi na Manda.
Makinda aliongeza
kuwa eneo la kijiji cha Mdilidili na Lugarawa lilitangazwa kwenye gazeti la
serikali namba 217 na kuchapishwa septemba 7 mwaka 2001 baada ya kupitia hatua
zote za kisheria.
Afisa ardhi alizitaja
changamoto zilizojitokeza katika mchakato huo kuwa ni pamoja na ongezeko la
ujenzi holela kwenye makazi ya watu,ongezeko la migogoro ya ardhi kwa ajili ya
shughuli mbalimbali kama uwekezaji, miundombinu na ugomvi wa mipaka na ardhi
huru kwa ajili ya huduma za jamii kama shule zahanati makaburi na nyumba za
ibada.
Changamoto zingine ni
ongezeko la watu wanaohitaji hati za viwanja, uvamizi wa ardhi kwenye vyanzo
vya maji, kukosekana kwa maeneo ya uwekezaji kama vile viwanda na biashara.
Makinda alizitaja
faida za kupima ardhi kuwa ni pamoja na wananchi kukatiwa hati miliki na
kuongezeka kwa thamani ya ardhi, kupunguza ujenzi holela na migogoro, kuwepo na
ardhi kwa ajili ya matumizi ya umma.
No comments:
Post a Comment